Wednesday 7 August 2013

ERICK KIMASHA ANASEMA TUMEONA YA FUTARI, TUSUBIRI YA KWARESMA

Tumeona ya Futari, Tusisubiri ya Kwaresma!

Ukistaajabu ya Musa, utayaona ya Firauni! Nilidhani kuwaona wanasiasa wanageuka waongoza Ibada ndiyo ingekuwa mwisho wa kustaajabu kwangu maishani. La hasha kumbe ndo bado kabisa vituko ndo viko arif!

Toka nizaliwe sijapa kuona tukio la kiibada lililogeuka kuwa msimu wa maonyesho ya kidunia kama Ramadhani ya mwaka huu. Sote tumemuona Rais wetu mkarimu wakiwafuturisha watu wake wa nguvu hususani wasanii, tumeona mabenki, makampuni ya simu na makampuni mengine yakifuturisha wateja wao, tumesikia Manispaa zikifuturisha, tumeona wabunge wengi tu wakitoa vitu vya kufuturisha katika majimbo yao, tusimsahau Mama Salma naye hakubaki nyuma. Wote hawa hawafuturu na walengwa ikabaki kuwa ibada yao ya sirini bali huakikisha pia uwepo wa vyombo vya habari kama sehemu kuu ya ibada yao. Na leo tunasoma habari za Edward Lowassa kufuturu Tanga. Nimevutiwa na Mtiririko huu wa jinsi matukio ya Kiibada yalivyogeuka majukwaa ya kisiasa na taratibu Wanasiasa wanavyozidi kujichukulia kiti kwenye mimbari na altare huku Wachungaji, Mashehe na Mapadri wakigeuka kuwa waumini na walei wakati waumini na walei wao wakichukua jukumu jipya ndani ya makanisa na msikiti kama washangiliaji. Nani ataliokoa kanisa la Mungu na wanyanganyi? Mtume gani atarudi kuzikomboa Masjid za mwenyezi Mungu?

Naamini katika matendo ya sadaka za kiibada lakini siamini katika show-off za namna ya ufuturishaji unavyofanywa. Naamini sadaka ya kweli ni ile mtu anayotoa moyoni si kwa ajili ya kuufamisha umma anafanya nini bali kwa ajili ya kumfurahisha muumba wake. Sote tumeona jinsi ufuturishaji ulivyogeuka kuwa sehemu ya CSR ya Makampuni na majukwaa ya kisiasa. Mwanzo miaka ya nyuma tulizoea makampuni ya simu ndiyo yalikuwa yanatumia ufuturishaji lakini sasa tumeona na wanasiasa wamevamia kwa kasi ya ajabu mlango huu. Kama mwenendo huu unahusiana na harakati za mwaka 2015, basi natabiri mwakani kuna wanasiasa na vyama vya siasa vitafuturisha mwezi mzima! Tutainajisi futari na itageuka chanzo cha kututenganisha. Wapo wataoanza kusema “mie nafuturu msikiti wa chama Fulani” na wengine watakuwa wanashiriki “futari ya mgombea fulani”

Tumebomoa misingi ya nchi, kila uchao tunavunja miiko ya vyama, tunahimiza na kutekeleza itikadi za kibaguzi, na baada ya kuharibu huko kote sasa tumevamia kuivunja misingi ya ibada za Mwenyezi Mungu?! Tutafakari upya tujirudi mapema. Tuwaambie hapana wanasiasa uchwara wanaotusababishia maisha magumu na njaa ili watuhadae kwa futari la msimu. Tutumie hekima na busara kuwakosoa viongozi wetu wa dini kwa kukumbatia ukengeufu wa namna hii kujongea patakatifu. Tusipofanya hivyo sasa, natarajia msimu ujao itakuwa zamu ya matukio haya haya kudurufiwa katika Kwaresma. Na ndipo katika madhehebu yote, tukio hili la ibada ya toba litakapokuwa limegeuka rasmi kuwa mateka na jukwaa la wanasiasa. Tumeona ya Futari, Tusisubiri ya Kwaresma kuchukua hatua!

Ni mtazamo wa Erick Kimasha, msomaji na mchangiaji wa hii Blog.

No comments:

Post a Comment