Zitto Akubali Kuvuliwa Unachama CHADEMA; Ahaidi Kurudi na Chama Kingine

Siku hii haikupaswa kufika huku; lakini imefika na historia inabakia historia. Zitto Kabwe aliyewahi kuwa Naibu Katibu Mkuu wa CHADEMA (Bara) amejivua uanachama (au amekubali kuvuliwa uanachama kulikotangazwa na CC ya chama) na hivyo kupoteza pia Ubunge wake. Wananchi wa Kigoma Kaskazini sasa hawana muwakilishi na hawatokuwa na mwakilishi kipindi kizima cha Bunge lililobakia (hasa Bunge la mwisho la Bajeti kabla ya Uchaguzi Mkuu).

Kauli yake mwenyewe katika kile ambacho kilitarajiwa kufanyika jana katika "Hotuba Niliyotaka Kutoa":

Mheshimiwa Spika, Kwa viongozi na wanachama wa CHADEMA, najivunia kwa fursa mliyonipa kuwa sehemu ya Baraza hili la Taifa ambalo leo ninalihutubia kwa mara ya mwisho kama mbunge wa Kigoma Kaskazini.

Inawezekana tusiweze kuelewana katika masuala ya uongozi, misingi na itikadi, lakini ninaamini tunapaswa kuelewana na kukubaliana katika dhamira kubwa ya kuijenga nchi yetu kuwa Taifa linalojitegemea na lisilo na aina yeyote ya ubaguzi. Taifa lenye uchumi shirikishi wenye kuzalisha ajira na kuondoa umasikini, ujinga na maradhi, yaani Taifa la Jamhuri ya Muungano wa Tanzania.

Na ni matumaini yangu kuwa tutakuwa bega kwa bega katika harakati hizi katika siku zijazo. Yaliyopita si ndwele tugange yajayo. Nafasi hii ya kihistoria tuliyopewa haihitaji siasa za ubinafsi na unafsi! Uzalendo wetu utapimwa kwa uwezo wetu wa kuweka tofauti zetu binafsi pembeni kwa lengo lililo kubwa zaidi yetu.
Na Barua yake ya kuondoka Bungeni:

Zitto Akubali Kuvuliwa Unachama CHADEMA; Ahaidi Kurudi na Chama Kingine
Ni wazi pia inaonekana tayari anaangalia chama kingine kujiunga nacho siku chache zijazo. Swali kubwa linabakia ni je hili litakuwa na matokeo ambayo baadhi ya watu wamekuwa wakiyakisia kuhusiana na kugawanya chama au nalo litapita?

Vyovyote vile ilivyo ni lazima tukubali kuwa yote yaliyotokea ni sehemu ya siasa zetu. Swali moja ambalo ameliibua na ambalo sisi kama taifa tunahitaji kulifanyia uamuzi mapema ni hili la kulazimisha wabunge kuwa wanachama wa vyama vya siasa na kuwa chama cha siasa kinaweza kumfutia mtu uanachama na akapoteza Ubunge wake. Ni lazima tutafute balance kati ya nidhamu ya chama (party discipline) na utumishi wa kisiasa. NI vizuri labda tuangalie namna ya kuweza kumfukuza mbunge Bungeni (hili lipo) bila kumfutia uanachama. Lakini kwenye Bunge ambalo lina wabunge wengi wa chama kimoja itakuwa Mbunge waupinzani akakubaliwa na Bunge la chama hicho lakini akashindwa kuondolewa na chama chake?

Ni muhimu kuwa na ubunifu wa aina fulani. Lakini pia sakata zima la Zitto linaacha tamanio moja la kutaka viongozi au wale wanaoitwa kuwa ni viongozi kujaribu kuonesha umakini wa kutatua migogoro mapema zaidi kabla haijafikia mafuriko.