Saturday 18 April 2015

Zitto Ajibu Tuhuma Za Kumchongea Mengi Kwamba Alichochea Wabunge Kuiangusha Serikali ya JK


Katika gazeti la Taifa Imara la tarehe 23 Machi 2015 kulikuwa na habari yenye kichwa cha maneno ' Zitto amchongea Mengi kwa JK?' Habari hiyo ilibeba maudhui ya 'post' iliyoandikwa katika mtandao wa Mwanahalisi online.
Habari hiyo inaonyesha kuwa Mimi nilikutana na Rais kwa msaada wa watu mbalimbali na katika kikao hicho inadaiwa nilisema kuwa Mengi ndiye aliyechochea wabunge kuishughikia Serikali ya Rais Kikwete ili ianguke.
Ni vema ifahamike kuwa gazeti la Taifa Imara linamilikiwa na Bwana James Rugemalira wa kashfa ya Escrow na kuendeshwa na Bwana Prince Bagenda aliye organise press conference ya mmoja wa mawaziri waliofukuzwa kazi kwa kashfa hiyo. Vile vile chanzo cha habari hiyo ni mtandao wa mwanahalisi online ambao unaendeshwa mmiliki wa Mawio gazeti ambalo kila wiki lina habari za kutunga dhidi yangu na chama cha ACT Wazalendo.
Habari hiyo ni ya kutunga yenye fitna zenye lengo la kuchonganisha watu. Naomba kufafanua ifuatavyo
1 Taarifa Maalumu ya Kamati ya PAC kuhusu ufisadi wa tshs 306 bilioni za Escrow hauhusiki na Bwana Reginald Mengi kwa namna yeyote ile. Mengi sio mbunge, sio mjumbe wa PAC na hakushawishi PAC kwa namna yeyote ile. Wezi wa Escrow wasitapetape kutafuta mchawi wakati mchawi ni wizi wao wenyewe. Porojo za kwamba Mengi alihonga wabunge ili kuishughulikia Serikali zinabaki porojo tu. Ila kama kuna mtu ana chembe ya ushahidi wa jambo hilo apeleke kwenye vyombo vya dola kwa hatua kuliko kurudia rudia porojo hizo kwenye vyombo vya habari.
2 Sihitaji kutumia watu ili kukutana na Rais Jakaya Kikwete kwani ninaweza kukutana naye kwa taratibu za kawaida kabisa za kiserikali. Hadithi ya kwamba nimeomba watu wanikutanishe na Rais inaonyesha namna mwandishi alivyoshindwa kutunga uongo wake. Katika kukutana kwangu na Rais kikazi sijawahi hata mara moja kuzungumzia watu. Hivyo kusema nilikwenda Ikulu kumzungumzia Bwana Mengi ni kunidharau na kuidhalilisha Taasisi ya Urais.
3 Nimemwelekeza mwanasheria wangu achukue hatua za kisheria dhidi ya Gazeti la Taifa Imara na vilevile Gazeti la Mawio kwa mfululizo wa habari za kutunga uongo dhidi yangu kila kukicha. Nimeagiza tupeleke mashtaka kwenda Baraza la Habari Tanzania ili magazeti hayo yathibitishe habari zao.
Zitto Kabwe
Kiongozi wa ACT Wazalendo.

No comments:

Post a Comment