Wednesday 15 January 2014

RC KAGERA ANAFICHA NINI?

MKUU wa Mkoa (RC) wa Kagera, Kanali mstaafu Fabiani Massawe, anafanya mbinu za kutaka kupindisha ukweli kuhusu tuhuma zinazomkabili Mstahiki Meya wa Manispaa ya Bukoba, Anatory Amani.
Manispaa hiyo imekumbwa na mgogoro mkubwa kati ya madiwani na meya huyo, vikao vya madiwani havikutani kwa zaidi ya mwaka. Suluhu imeshindikana hadi kufikia hatua ya kuletwa Mdhibiti na Mkaguzi Mkuu wa Hesabu za Serikali (CAG), Ludovick Utouh, ili akague miradi inayolalamikiwa.
Wakati ripoti ya CAG ikisubiriwa iseme kilichobainika, mkuu wa mkoa anajaribu kutumia njia za panya kutaka kumaliza mgogoro huo kwa mbinu za kijanja.
Huku akielewa wazi kwamba madiwani wamechaguliwa na wananchi na hivyo wanawajibika kwao, Massawe anaamua kuitisha kikao alichokiita cha usuluhishi ili kuwashawishi wakubali kuketi na ‘mtuhumiwa’ kupitisha bajeti ya 2014/2015.
Massawe anajificha kwenye migongo ya viongozi wa dini, Askofu msaidizi wa Jimbo Katoliki la Bukoba, Methodius Kilaini, Sheikh wa Wilaya ya Bukoba, Haruna Kichwabuta na wazee maarufu ili wamsaidie kuwalainisha madiwani, lakini anagonga mwamba.
Madiwani hao wanane wa CCM wanaompinga meya pamoja na wale saba wa upinzani, wanamshangaa Massawe na viongozi wake wa usuluhishi kuwa walikuwa wapi mwaka mzima wakati mgogoro huo ukiendelea.
Wanahoji kwanini asubiri hadi ripoti ya CAG inakaribia kuletwa mezani ndipo anazunguka kuwalainisha ili wapitishe bajeti upesi, tena kwa vitisho na ubabe kwamba watakaogoma kuhudhuria watafukuzwa udiwani.
Tunahoji kwa Massawe tukitaka kufahamu hasa analenga kuficha nini katika mgogoro huo wa Bukoba. Kwanini awe na haraka wakati ripoti ya CAG yenye ukweli wote iko tayari?
Kama naye sio sehemu ya ufisadi huo, ni kwanini asingoje CAG aiwasilishe ripoti ili isomwe na mchawi wa maendeleo ya Bukoba ajulikane kama ni madiwani au meya na viongozi wa serikali?
Mgororo wa Bukoba haukuanza juzi wala jana, viongozi wa dini pamoja na hao wazee wanaojaribu kutumiwa na Massawe, lazima watiliwe shaka kwamba walikuwa wapi tangu viongozi wote wa juu wa CCM akiwemo Rais Jakaya Kikwete wanashindwa kuutatua hadi kuomba CAG awatafutie ukweli?
Sasa kama ukweli huo uko tayari, kwanini Masaswe anajaribu kuzunguka mlango wa nyuma ili wananchi wasijue CAG alibaini nini? Katika jitihadi hizi za udalali wa kujaribu kumkinga Meya Amani, mkuu wa mkoa ana maslahi gani?
Kwa kitendo alichokifanya Massawe juzi, ni wazi kuwa amewadharau viongozi wa CCM na mkuu wake, yaani Rais Kikwete kwa kuingilia suala ambalo uamuzi wake ulikwishapelekwa kwenye ngazi nyingine.
Massawe ameletwa kuiongoza Kagera kama mteule na ataiacha wakati wowote mteule wake atakapoamua vinginevyo, sasa ni kwanini hawapi nafasi wawakilishi halali wa wananchi (madiwani) wakatimiza majukumu yao kwa kuzingatia utaratibu unaofaa?

No comments:

Post a Comment