Monday 16 September 2013

TEC yataka Kamishna wa Polisi Z’bar afukuzwe kazi


Padri Joseph Magamba wa Kanisa Katoliki Parokia ya Machui Zanzibar aliyemwagiwa tindikali akisaidiwa kushuka kwenye ndege na Padri Thomas Assenga(kushoto) wa Kanisa la Mtakatifu Joseph Zanzibar baada ya kuwasili kwenye uwanja wa Julius Nyerere Dar es Salaam jana kuelekea katika hospitali ya Taifa Muhimbili kwa matibabu zaidi
  • Yadai ameshindwa kuwakamata watuhumiwa wanaowamwagia  tindikali viongozi wa dini.

Dar es Salaam. Tukio la kumwagiwa tindikali  Padri wa Kanisa la Romani Katoliki Parokia ya Machui, Joseph Mwang’amba huko Zanzibar limechukua sura mpya baada ya  Baraza la Maaskofu wa Katoliki Tanzania (TEC) kumtaka Kamishna wa Polisi Zanzibar, Mussa Ali Mussa kufukuzwa kazi.
Makamu  Rais wa TEC, Askofu Severine Niwemugizi aliliambia gazeti hili jana kuwa anapaswa kuondolewa kwa sababu ya kukithiri kwa matukio hayo visiwani.
Askofu Niwemugizi alisema kamanda huyo anapaswa kuchukuliwa hatua kwa kuwa ameshindwa kukamata watu wanaofanya vitendo viovu dhidi ya viongozi wa dini.
Kwa upande wake Kamishna Mussa alisisitiza hawezi kujiuzulu na kwamba anayestahili kulaumiwa ni Mkurugugenzi wa Mashitaka (DPP) kwa sababu kwa upande wake alishawakamata watuhumiwa wa matukio hayo.
“Kazi yangu mimi ni kupeleleza na kukamata watuhumiwa,ila kazi ya kushitaki watu ni ya DPP hivyo mimi siyo wa kulaumiwa’Alisema .
Hili ni tukio la nne la uhalifu dhidi ya viongozi wa dini huko Zanzibar baada ya kuuawa kwa Padri Evarist Mushi wakati Padri Ambrose Mkenda alipigwa risasi na Katibu wa Mufti, Sheikh Fadhili Soraga alimwagiwa tindikali.
  Katika hatua nyingine, Askofu Niwemugizi alisema kuwa matukio hayo kwa sasa yamekuwa wazi kwamba ni mpango wa kuangamiza Ukristo na Wakristo kwa ujumla katika Visiwa vya Zanzibar.
“Uchochezi umefanywa wa kuhamasisha chuki dhidi ya Ukristo unasikitisha. Tulikaa kama Wakristo tukaiambia Serikali mambo ambayo inaweza kufanya kukomesha vitendo hivi, lakini hadi sasa hakuna lililotekelezwa,” alisema na kuongeza: 
“Awali ilielezwa kwamba siyo sababu ya kidini,  watu wa Kikundi cha Uamsho ndiyo walioanzisha moto huo na wanauendeleza, hali inatisha zaidi kwamba hata jamii ya Wazanzibar haionyeshi nia ya kushiriki kukomesha ukatili huu, kama huyu Padri Mwang’amba amemwagiwa kwenye kituo cha intaneti ni eneo ambao lina watu mbona mhusika hajakamatwa? alihoji.
Wakati huohuo, Mwenyekiti wa Kamati ya Haki na Maadili kwa Jamii kwa Viongozi wa Dini ya Kikristo, Mchungaji William Mwamalanga alisema kuwa Kamishna huyo wa Polisi anatakiwa kufukuzwa kazi kwa kuwa anaichafua Zanzibar kwa kushindwa kudhibiti matukio hayo ya uhalifu kwa makusudi, pia amejaa udini.

No comments:

Post a Comment