Friday 29 November 2013

FIFA WAFUNGUKA BAADA YA UWANJA WA KOMBE LA DUNIA KUPOROMOKA BRAZIL



SHIRIKISHO la Kimataifa la Mpira wa Miguu (Fifa) imesema halina mpango wa kuhamisha michuano ya Fainali ya Kombe la Dunia 2014 kutoka nchini Brazil ingawa nchi hiyo imepata changamoto katika maandalizi ya michuano hiyo.
Wafanyakazi wawili walipoteza maisha baada ya kuangukiwa na nguzo ambazo ziliharibu uwanja wa Corithians ulio mjini Sao Paulo.
Timu ya taifa ya Brazil inatarajiwa kucheza mechi ya ufunguzi ya Kombe la dunia katika uwanja huo wenye uwezo wa kuwa na watazamaji 65,000.
Vyanzo vya habari vya juu ndani ya Shirikisho hilo vimeendelea kusisitiza kuwa hakuna mbadala kutokana na kutokea kwa ajali hiyo.
Brazil ilikiri kuwa inafanya jitihada za kumaliza ujenzi wa viwanja 12 kwa ajili ya michuano hiyo, sita kati ya hivyo ipo tayari kwa ajili ya michuano ya kombe la shirikisho.
Ajali iliyotokea siku ya Jumatano ni ya tatu kusababisha kifo katika viwanja vitakavyopigiwa kipute cha kombe la dunia. Wafanyakazi wengine wawili walipoteza maisha kipindi cha miaka miwili iliyopita.

Uchunguzi umeanza hii leo kubaini chanzo cha ajali mjini Sao Paulo.

No comments:

Post a Comment